Tamwa yataja chanzo cha mimba za utotoni

CHAMA Cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kimewataja wabunge na madiwani kuwa chanzo cha wanafunzi wa kike kupata mimba shuleni.

Hayo yalielezwa na mkurugenzi mtendaji wa Tamwa, Ananilea Nkya alipokuwa anaoa ripoti ya utafiti kuhusu mimba mashuleni kwenye mikoa 17 nchini.

Alisema wawakilishi hao ni sababu za kukithiri mimba mashuleni kwa kuwa hawazitembelei shule hizo na kujua matatizo yake, kisha kujenga hoja kwa mamlaka husika ili wazifanyie maboresho.

Nkya alisema viongozi hao wangeweza kujenga hoja katika vyombo vyenye mamlaka za kutenga fedha ambavyo ni Halmashauri na bunge ili hatua sahihi ziweze kuchukuliwa.

“Utafiti uliobaini baadhi ya watoto wa kike wa shule waliopata ujauzito na kukatisha masomo walidanganyika kwa kupewa chakula kutokana na kushinda njaa kuanzia asubuhi hadi jioni wakiwa shuleni,” alisema Nnkya.
 
Nkya alisema wengine waliopata ujauzito walidanganyika kwa kupewa msaada wa usafiri kutokana na shule kuwa mbali na makazi ya watu hivyo tulibaini kuwa wanafunzi wengi wanatembea umbali mrefu hadi kilometa 20 kwenda shule.

“Tatizo la shule kuwa mbali lingeweza kuepusha mimba iwapo shule zingekuwa na mabweni kwa ajili ya wanafunzi wanaoishi mbali na shule,”alisema.

Alisema mfumo wa elimu ubadilike gharama ya elimu itoke katika mfuko wa serikali zisitumike fedha za wazazi hivyo kila mtoto wa kike na kiume wanatakiwa wapate elimu bure.

“Mtoto amefaulu anatakiwa aende shule mkoani inatokea mzazi wakuwa hawana fedha ya kumsafirisha na kumlipia ada anaona bora amuache motto wa kike matokeo yake anashika mimba ya utotoni au anaolewa akiwa mdogo,”alisema Nkya.

Kwa mujibu wa taarifa za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi katika kipindi cha mwaka 2004 hadi 2008, jumla ya wanafunzi 28,590 wakiwepo 11,599 wa sekondari na 16,991 wa shule za msingi walikatishwa masomo kwa kupata  mimba.

Nkya alisema taarifa zinaonyesha kuwa katika shule za sekondari mimba shuleni  matukio ya mimba yalikuwa 772 mwaka 2004 lakini yaliongezeka na kufikia 4,965 kwa mwaka 2008.

Mikoa iliyofanyiwa utafiti ni Dar es Salaam, Morogoro, Iringa, Mbeya, Dodoma, Kigoma, Mwanza, Mara, Shinyanga, Tanga, Kilimanjaro, Tabora, Lindi, Ruvuma, Manyara Kaskazini Pemba na Kusini.

Source Mwananchi -posted  Sunday, October 3  2010 at  00:00

No comments: