Vijana, nguvukazi inayotumika visivyo(Young people Mis-used)


Na Joyce Mmasi-Mwananchi
VIJANA ni taifa la kesho. Huu ni msemo  wa zamani uliozoeleka na hutumiwa zaidi na wanasiasa, wakiwa na lengo la kuwaweka vijana nyuma wakisubiri kesho isiyofika.
Idadi kubwa ya vijana ndio inayoonekana kuleta hamasa katika siasa nchini. Vijana ndio wanaoviwezesha vyama mbalimbali kuonekana kuwa na nguvu na vyenye hamasa.
Lakini vijana hao hao ambao wamekuwa wakionekana kuvisaidia vyama vya siasa, wanakabiliwa na matatizo mbalimbali yakiwamo ukosefu wa ajira, matumizi ya dawa za kulevya, na ushiriki hafifu katika masuala ya kijamii yatakayowaletea maendeleo.
Viongozi wa kisiasa kwa ujumla wao kwa nyakati tofauti huonyesha umahiri katika kuyaeleza matatizo ya vijana lakini hakuna mwanasiasa wala chama ambacho kimeweza au kuonyesha njia ya kuyatatua.
Hisia iliyojengeka miongoni mwa baadhi ya vijana wenyewe, ni kuwa matatizo yao yamekuwa yakiachwa yaendelee kuwapo, na si kweli kwamba hayatatuliki, kwa kuwa wenye mamlaka wa hofu, kuwa vijana wakiwa na shughuli ya kufanya na uwezo kiuchumi, ni vigumu kuendelea kuwatumia na huenda wataikosa nguvu ya katika shughuli za kisiasa.
Hii inatokana na dhana kuwa vijana wengi wanaojitokeza kushiriki maandamano, na mikutano ya hadhara ya kisiasa hufanya hivyo kutokana na kukosa kazi za kufanya.
Idadi kubwa ya vijana tangu wale waliomaliza ngazi mbalimbali za elimu, kama ile ya shahada, stashahada, vyeti na hata wale ambao hawajapata elimu yoyote, wanakabiliwa na ukosefu wa ajira na kujikuta wakijiingiza katika makundi yasiyofaa.
Mbali na kukosa ajira, wapo vijana wanawake kwa wanaume ambao wamejikuta wakijiingiza katika vitendo visivyofaa kama matumizi ya dawa za kulevya, ukahaba, ushoga, usagaji na makundi mengine yasiyofaa na kusababisha kero na wakati mwingine kutengwa na jamii.
Siasa imeoneka kuwa suluhisho kwa vijana wengi kudhani kuwa watetezi wao ni wanasiasa wanaowataja katika mikutano yao.
Kila kijana asiye na ajira, na wakati mwingine aliyeathirika na vitendo visivyofaa hukimbilia kujiunga mkono vyama vya siasa na kuvishabikia ,huku wakibaki kusubiri sera zao nzuri za kuwakomboa na kuwapatia ajira.
Lakini miaka inapita na hakuna suluhisho lililopatikana kwa vijana. Wengi wameendelea kukua na wengine kuvuka umri wa ujana wakiendelea kuwa maskini na wasio na maendeleo zaidi ya kuzama katika dimbwi la umaskini.  
Kutokana na tatizo hili kuonekana kuwa kubwa na sugu, baadhi ya vijana wanafunzi kutoka vyuo vikuu nchiniwameungana na kuunda umoja wao wenye lengo la kusaidia kutafuta ufumbuzi wa matatizo yanayowakabili vijana nchini.

No comments: